MAKALA: KUTANUA WIGO WA MATUMIZI YA LUGHA YA KISWAHILI KATIKA NYANJA ZOTE

                                          Source: Global TV


UMUHIMU WA KISWAHILI KATIKA NYANJA ZA KITAALUMA
Na Jennifer Walter

Lugha ya Kiswahili ni lugha ambayo imevuka mipaka ya ukabila na utaifa. Ni lugha ambayo inakua na kuenea kwa kasi. Kukua kwa lugha hupimwa kutokana na mawanda mapana ya utumizi pamoja na kuongezeka kwa idadi kubwa ya watumiaji.

Mwenye masikio na asikie, mkataa kwao mchawi. Kuna baadhi ya wasomi  hudharau lugha ya Kiswahili kwa kuiona ni lugha ya hadhi ya chini. Tunatakiwa kuelewa kuwa hakuna lugha yoyote dunani ambayo ni bora kuliko lugha nyingine. Lugha yoyote ni bora kwa kuwa inakidhi haja ya mawasiliano miongoni mwa watumiaji.

Pengine lugha hii ya Kiswahili inadharauliwa kutokana na kutojulikana asili yake ni wapi. Bado kuna mjadala mkubwa na endelevu kuhusu asili ya lugha ya Kiswahili. Wataalamu hao huibuka kwa hoja  mbalimbali na kutetea madai yao. Wapo wanaodai kuwa Kiswahili asili yake inatokana na lugha ya Kiarabu, ya Kibantu, mchanganyiko wa lugha ya Kiarabu na Kibantu, Kibantu kilichochanganyika na Kiarabu na mchanganyiko wa lugha mbalimbali za Kibantu  kutoka upwa wa Afrika Mashariki.

Jambo la ajabu zaidi ni kuwa hata Mswahili mwenyewe bado hajulikani ni yupi!  Wako baadhi ya watu ambao hawependi kuitwa Waswahili kwa kuwa maana ya Mswahili inaandamana na sifa mbaya mathalani mtu laghai, mwenye hadhi ya chini kiuchumi, asiyejali muda, kutumia maneno mengi kujieleza au kujitetea n kadhalika.

Tunawezaje kuwaachia wageni kupata fursa zitokanazo na lugha ya Kiswahili ilhali wenyewe tumerudi nyuma? Wageni wajapo kwetu kujifunza Kiswahili na hupenda kukitumia ili kuwasiliana na wenyeji, lakini sisi kwa kujidai tunajua tunazungumza nao kwa kutumia lugha zao. Mgeni huyu akibobea katika Kiswahili tutaweza kushindana naye katika soko la ajira?

Wanaodhani wanaelewa Kiswahili ndio wa kwanza kukosea na kukiharibu. Wageni wanajua Kiswahili pengine kuwashinda wazawa kwa kuwa wao hufuata kanuni sahihi za kisarufi wakkati wenyeji kuongea Kiswahili cha mazoea chenye makosa mengi. Baadhi ya makosa ni kama vile ‘ilikusudi’. Kwa mfano, “Nimekuja ili kusudi niwasaidie”. Ili na kusudi ni maneno yenye hadhi sawa yanayoelezea sababu, hivyo hayatakiwi kutumika pamoja. Mfano mwingine ni “Mimi binafsi”. Mfano huu wa “mimi binafsi nitachangia laki mbili”. Mimi ni kiwakilishi cha binafsi hivyo unatakiwa kuteua neno moja litumike badala ya maneno mawili.

Tunatakiwa tuelewe kwamba vyuo vikuu vingi duniani vinafundisha lugha ya Kiswahili; mathalan Chuo Kikuu cha Egerton, Kenyatta, nk huko Kenya, Cambridge, Edinburgh  huko Uingereza, Columbia, Philadelphia, nk huko Marekani na vingine vingi.

Profesa Sun Baohua wa Chuo Kikuu cha Lugha za Kigeni cha Beijing (CRI) anaeleza kuwa “Somo la Kiswahili hufuata utaratibu wa kufundisha kwa miaka minne. Miaka miwili ya kwanza tunaiita kipindi cha kuwawekea msingi wanafunzi ambapo tunafungua somo rasmi la Kiswahili, somo la kuzungumza, kusikiliza na somo la ziada. Miaka miwili ya pili tunaiita kipindi cha kuinua uwezo wa lugha. Wanafunzi wanatakiwa kufundishwa somo la  uandishi wa habari, ukalimani, tafsiri, fasihi ya Kiswahili na somo la  taarifa za habari kutoka nchi ya Afrika Mashariki”.

Walimu wa kufundisha lugha ya Kiswahili katika vyuo hivyo wapo wachache. Wataalamu wa ukalimani na tafsiri nao wanahitajika zaidi ili kuzidi kueneza lugha hii. Wataalamu wa lugha ya Kiswahili hawapatikani katika vitivo au ndaki nyingine isipokuwa katika kitivo cha Kiswahili.

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinapokea wanafunzi wachache wanaochukua kozi za Kiswahili na wengine kuhama. Kwa mfano mwaka huu (2016) wamehitimu wanafunzi 18 tu wa shahada ya awali ya Kiswahili. hata hivyo viko vyuo vingine Tanzania ambavyo hufundisha Kiswahili kwa digrii ya kwanza nay a uzamili kama vile Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo Kikuu chaTumaini Makumira Arusha, Ruaha, Iringa na Chuo Kikuu cha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SUZA).

Kipi kifanyike ili kuwapata wataalamu wengi wa Kiswahili? Elimu kwa wanajamii inatakiwa kutolewa ili jamii  itambue umihimu na fursa zipatikanazo katika lugha ya Kiswahili. Wanajamii wakikombolewa kifikra tutapata wanafunzi wengi kutokana na wanajamii kuhamasika juu ya thamani ya lugha ya Kiswahili. Kiswahili kwa sasa ni kisima cha mafanikio kwani wapo wanaokula, wanaolala na kuishi kutokana na  lugha ya Kiswahili. Suala la ukosefu wa ajira kwa vijana litapungua kwa kuwekeza katika lugha adhimu ya Kiswahili.

Kupenda lugha yetu ni pamoja na kuiongea mfululizo bila ya kuchanganya na lugha nyingine. “Longa Kiswahili ujisikie huru” ni moja ya kauli mbiu ya kongamano la Chama cha Wanafunzi wa Kiswahili Vyuo Vikuu Afrika Mashariki (Chawakama) kilichoanzishwa mwaka 2004 kwa lengo la kukuza Kiswahili kwa wanafunzi wanaosoma lugha ya Kiswahili vyuoni.

Kusisitiza matumizi ya Kiswahili katika sekta zote za serikali, sekta za watu binafsi na mashirika ya umma ikiwa ni pamoja na kutumia  mawasiliano kwa maandishi kwa barua zote za kikazi ili kukikuza Kiswahili. Serikali inatakiwa kutunga na kusimamia sera zitakazoboresha na kukuza zaidi lugha ya Kiswahili.

Katika kutekeleza jukumu hili, Taasisi ya Taaluma za Kiswahili (Tataki) chini ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam imeandaa vitabu vya masomo yote ya shule ya sekondari kuanzia na kidato cha kwanza yakiwamo masomo ya sayansi na Huisabati kwa lugha ya Kiswahili. Katika kukuza lugha na kuboresha mfumo wa elimu nchini, serikali haina budi kuutazama mradi huu kwa jicho la tatu kwani kwa kufundisha lugha ya Kiswahili katika shule za sekondari kutainua lugha ya Kiswahili na kukuza viwango vya ufaulu nchini.

Comments