HABARI: KUKATIKA KWA UMEME DAR KWAMUANGAMIZA MFANYAKAZI WA TANESCO

ALHAMISI OKTOBA,3 2019
 Waziri wa Nishati nchini Tanzania, Dk Medard

Waziri wa Nishati nchini Tanzania, Dk Medard Kalemani  

Kwa ufupi:

Waziri wa Nishati nchini Tanzania, Dk Medard Kalemani amemsimamisha kazi muongoza mifumo ya umeme wa kituo cha kupoza nishati hiyo cha Ubungo jijini Dar es Salaam, Samson Mwangalume.
____________________________________________________________
Dar es Salaam. Waziri wa Nishati nchini Tanzania, Dk Medard Kalemani amemsimamisha kazi muongoza mifumo ya umeme wa kituo cha kupoza nishati hiyo cha Ubungo jijini Dar es Salaam, Samson Mwangalume.
Amechukua uamuzi huo leo Alhamisi Oktoba 3, 2019 baada ya usiku wa kuamkia leo umeme kukatika huku chanzo kikielezwa kuwa ni uchafu wa vikombe katika njia za kusafirisha nishati hiyo.
Dk Kalemani pia ametoa onyo la mwisho kwa kaimu meneja mwandamizi wa usafirishaji wa umeme, Amos Kahiyula kuhakikisha haukatiki kutokana na uzembe.
Ametoa maagizo mara baada ya kutembelea kituo hicho na kutoridhishwa na maelezo ya Kahiyula aliyetoa sababu hizo baada ya kutakiwa na waziri huyo kueleza chanzo.
"Haiwezekani watu mkae muda mrefu bila kutazama hali ya vikombe hadi viwe vichafu kiasi cha kusababisha umeme kukatika, huu ni uzembe usiokubalika kwani serikali imeshawekeza vya kutosha kuhakikisha umeme unakuwa wa uhakika.”
" Nataka huyo Samson aliyekuwa mkuu wa zamu asimamishwe kazi kuanzia leo na maelezo yake niyapate leo ofisini kwangu  kwani kama ni vikombe vipo kwa nini hamkuviweka,” amesema Dk Kalemani.
Ameongeza, “Pia tulishatoa nyumba kwa wafanyakazi katika kituo hiki  ili iwe rahisi kufika kwenye mitambo kunapotokea tatizo lakini hakuna hata mmoja anayekaa na badala yake mnakaa majumbani kwenu na kusababisha wengine kutembea hadi kilometa nne kufika hapa.  Hii  haikubaliki.
Kutokana na hilo, amesema mpaka saa nane mchana leo  wafanyakazi sita waliopewa nyumba katika kituo hicho wahamie kwa kutumia magari ya Tanesco.

Na Nasra Abdallah, Mwananchi nabdallah@mwananchi.co.tz


Comments