MAKALA: JIFUNZE LUGHA YA KISWAHILI/LEARN SWAHILI LANGUAGE




___________________________________________________________

UMUHIMU WA KISWAHILI KATIKA TAIFA
    

Mwalimu J. K. Nyerere ametuasa tusiwe wabinafsi katika masuala yahusuyo taifa. Suala la ubinafsi amelipiga vita tangu alipoasisi taifa hili na kutuagiza tuondokane na unafsi kama alivyoandika katika kitabu chake cha ‘Tujisahihishe.’ Kitabu hiki kilichapishwa mwezi Juni 1962. Kwa maana hiyo, alitupa fursa ya kuielimisha jamii bila uchoyo na husuda.
Katika eneo la lugha, tunayo mambo mengi tunayoweza kujifunza kwa faida yetu binafsi, kwa taifa letu na kwa ulimwengu mzima kwa jumla. Hapa yafaa nitoe ufafanuzi kidogo.  Katika miezi ya hivi karibuni liko jambo lililotokea huko Uingereza ambalo ni mfano wa kuigwa.
Wabunge wa Bunge la Uingereza ambao ni wapenzi wa lugha yao ya taifa hawakuridhishwa na hadhi ya lugha yao inavyotumika kitaifa na kimataifa. Wameishauri  Serikali yao iimarishe ufundishaji wa lugha ya Kiingereza katika shule zote na hasa  vyuo vya lugha. Pia waliishauri serikali kufundisha Kiingereza kwa umakini mkubwa katika shule na vyuo. Pia walishauri kuwa shule na vyuo vya lugha viongezewe fedha katika bajeti kila mwaka ili  kupatiwa fedha mwaka hadi mwaka kuanzia mwaka 2011/2012. Pamoja na kutilia mkazo mafunzo ya lugha yao, wamesisitiza pia lugha za kigeni zisomeshwe kwa watu wa kada mbalimbali hasa  wanadiplomasia.
Kamati ya Mambo ya Nje ya Bunge imeshauri kuwa kupandishwa vyeo kwa maofisa kutokane na ujuzi na weledi wa Kiingereza pamoja na lugha moja ya kimataifa.     Wamekubali bajeti kwa mafunzo ya lugha iongezeke kutoka $ 3 milioni kwa mwaka 2011/12 hadi $ 3.9 milioni kwa mwaka 2013/14. Vilevile idadi ya wanafunzi kwa mwaka iongezwe na kuwa 1000.
 Lugha kubwa za nchi za nje kama lugha ya Mandarin, Kiarabu, Kihispania na Kireno zisomeshwe shuleni. Lugha ya Mandarin ni lugha rasmi na lugha ya taifa la Wachina. Lugha ya Kihispania hutumika katika nchi za Argentina, Chile, Uruguay, n.k.  Kireno hutumika katika nchi za Brazil, Cuba, Venezuela, n.k  Kireno. Nchi za  Argentina, Chile, Uruguay, n.k.  hutumia   Kihispania.  Lugha hizi mbili hutumika katika nchi za Amerika ya Kusini. Lugha ya Kiarabu nayo inatiliwa mkazo kama lugha muhimu na sababu kubwa ni za kiuchumi na kisiasa.
Je, Waingereza wamegundua nini walipoamua kufungua tena chuo chao cha lugha walichofunga mwaka 2007? Bila shaka wamegundua kuwa nafasi ya lugha ni kubwa duniani hasa katika mazingira ya utandawazi kama masuala ya diplomasia, biashara, siasa na uchumi. Uamuzi wa kujifunza lugha ya Kiarabu, Kimandarin, Kihispania na Kireno ni kuwawezesha Waingereza kujua kwa undani masuala mengi yanayowahusu Wachina, nchi  za Amerika ya Kusini na Waarabu katika biashara. Kwa upande wa Kiarabu ni dhahiri kuwa ni suala la mafuta.
Katika bara la Afrika, ziko lugha tofauti ambazo zinatufanya tusielewane kutokana na sababu za kihistoria. Nchi za Afrika zinatumia lugha zenye asili ya kikoloni kama Kiarabu, Kifaransa, Kireno na Kiingereza. Hizi ndizo lugha zinazotumika katika vikao vya Umoja wa nchi za Afrika (AU)
Lugha ya Kiafrika iliyokubaliwa kutumika katika shughuli za kikazi za AU ni Kiswahili. Tanzania ilipewa jukumu la kukikuza na kukiendeleza Kiswahili ili kifikie hadhi ya Kimataifa. Agizo hili lilitolewa mwaka 1988 huko Addis Ababa, Ethiopia.Tumefikia wapi tangu mwaka 1988  Tanzania ilipoteuliwa katika kikao kilichofanyika huko Mauritus cha Mawaziri wa Umoja wa Nchi huru za Afrika (OAU) na kuridhiwa na Wakuu nchi na serikali mwaka huo huo? Ilitakiwa uandaliwe utaratibu  wa mafunzo ya ukalimani na tafsiri kwa ajili ya kuwaandaa wataalamu kwa kazi katika Umoja wa Nchi Huru za Afrika.
Mafunzo yaliandaliwa kwa kuwapeleka wataalamu wazalendo waliozifahamu lugha za Kifaransa, Kiingereza na Kiswahili.  Wataalamu hawa walipelekwa Chuo Kikuu cha Paris kwa kipindi cha mwaka mmoja. Baada ya kufaulu walirejea nyumbani llakini hawakuelekezwa kujiandaa kwenda Addis Ababa. Mpaka leo mpango wa kwapeleka Watanzania Addis Ababa haukutekelezwa kikamilifu.
Kwa suala la ukuzaji wa Kiswahili ndani ya nchi, mipango   imekwama ya kukuza Kiswahili kutokana na kutokuwepo kwa sera ya lugha iliyo wazi. Kila waziri mwenye dhamana ya kusimamia lugha anapoteuliwa huwa hana mawazo ya kutupeleka mbele katika kukifanya Kiswahili kiwe ni lugha imara ya kitaifa.
Hapa nchini kiko kituo cha kufundisha lugha za kigeni  huko Zanzibar linachojulikana kama Taasisi ya Kiswahili na Lugha za Kigeni (TAKILUKI). Kina kila sababu ya kuitwa kituo cha lugha kwani kinafundisha  lugha za kigeni kama  Kiarabu, Kiingereza , Kijerumani na Kifaransa katika ngazi ya Diploma kikiwaandaa wataalamu wa ngazi ya kati. Pia kinafundisha Kiswahili kwa wageni wanaokuja hapa nchini ama kufanya kazi au kujifunza Kiswahili ili baadaye wakafundishe katika nchi zao.
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itambue kuwapo kwa kituo hiki na kipatiwe fedha za kutosha. Yanatakiwa  maboresho ya hali ya juu ili kukiwezesha kituo hiki kikidhi vigezo vya kimataifa. Kwa mfano wanatakiwa wahadhiri wenye digrii za uzamili na uzamivu katika lugha nilizotaja hapo juu pamoja na vifaa vya kufundishia kama vitabu, video na kanda zake na vilevile maabara kisasa za lugha kwa ajili ya kufundishia fonetiki, fonolojia na sintaksia.
Kituo hii kitawavutia wanafunzi wengi kutoka nje na  taifa litapata fursa nzuri ya kujiongezea kipato pamoja na kuwaandaa Watanzania ujipatia ajira nchi za nje.
Na Stephen Maina    

____________________________________________________________


Faida ya lugha ya Kiswahili kwa Watanzania nchi za SADC

Baadhi ya viongozi wa SADC
Mpaka sasa Kiswahili ni miongoni mwa lugha rasmi katika Jumuiya za Kikanda ambazo ni Umoja wa Afrika na Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kwa upande wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kiswahili kitasambaa na kuhamasisha wakazi wa nchi ya Sudan ya Kusini ambao wamejiunga hivi karibuni kujifunza lugha hiyo.

AGOSTI 17 hadi 18 mwaka huu, Tanzania ilipata fursa ya kuwa wenyeji wa Mkutano wa 39 wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), ambapo Rais Dk. John Magufuli alikabidhiwa uenyekiti wa jumuiya hiyo.

Hiyo ilikuwa fursa nyingine ya Tanzania kupokea kijiti cha uongozi tangu mwaka 2003.
Kikao hicho cha siku mbili kilitanguliwa na vikao mbalimbali huku asasi za kiraia, viongozi wa dini, wafanyabiashara na wafanyakazi, walipeleka maoni yao kwa viongozi wananchi za SADC kwa lengo la kupewa kipaumbele katika mazungumzo ya kikao.

Katika mambo yaliyozungumziwa na kuwasiliishwa na makundi hayo hususani kutoka Tanzania, ilikuwa ni matumizi ya lugha ya Kiswahili katika jumuiya hiyo.

Maoni ya kutumia lugha ya Kiswahili katika Jumuiya ya SADC, yaliendelea kuwekewa mkazo na Rais Magufuli katika kikao cha wakuu wa nchi. Mkutano wa viongozi wa SADC ulikamilika kwa maazimio kadhaa ikiwemo kuidhinisha lugha ya Kiswahili kuwa lugha rasmi ya nne itakayotumika katika shughuli za jumuiya hiyo.

Matumizi ya lugha ya Kiswahili katika SADC ni wazi kwamba itakuza lugha ya Kiswahili katika nchi 15 wanachama wa Jumuiya ya SADC ambazo ni; Zimbabwe, Msumbiji, Angola, Zambia, Botswana, Malawi, Lesotho, Swatini, Afrika ya Kusini, Madagaska, Mauritius, Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Seychelles, Namibia na Comoro.

Uamuzi wa kuidhinisha matumizi ya Kiswahili kuwa lugha rasmi ya nne katika Jumuiya ya SADC ni hatua kubwa kwa historia ya maendeleo ya lugha ya Kiswahili na utamaduni wa kitanzania.

Mpaka sasa Kiswahili ni miongoni mwa lugha rasmi katika Jumuiya za Kikanda ambazo ni Umoja wa Afrika na Jumuiya ya Afrika Mashariki. Kwa upande wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kiswahili kitasambaa na kuhamasisha wakazi wa nchi ya Sudan ya Kusini ambao wamejiunga hivi karibuni kujifunza lugha hiyo.

Ni wazi kwamba, Watanzania na baadhi ya nchi za SADC zinazotumia lugha ya Kiswahili kama Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Malawi na Zambia watanufaika kama watangulizi na wataalamu wa lugha ya Kiswahili ikilinganishwa na wanachama wengine wa SADC.

Mkataba wa SADC unaainisha malengo makuu ya kuanzishwa kwa jumuiya hiyo ikiwemo kukuza umoja, amani na usalama katika mtengamano wetu.

LUGHA KAMA HAKI

Matumizi ya lugha ya Kiswahili yatahakikisha na kuchochea ufikiwaji wa haki ya ushiriki wa wananchi katika masuala ya maendeleo. Mathalani ibara ya 21(2) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inatoa haki na uhuru kwa kila raia kushiriki kikamilifu katika mchakato wa maamuzi katika mambo yanayomhusu au kumuathiri. Hivyo basi, Watanzania ambao wengi wao ni wazungumzaji wa lugha ya Kiswahili, wataweza kuelewa na kushiriki kwa namna tofauti mambo yatakayofanyiwa maamuzi na Jumuiya ya SADC.

UMUHIMU WA LUGHA YA KISWAHILI

Katika mawanda ya kimataifa lugha ya Kiswahili inazungumzwa na watu zaidi ya milioni 150 duniani na kwa Afrika Kiswahili kikiwa ni lugha ya kwanza ya asili inayozungumzwa na watu wengi. Kwa Afrika, Kiswahili kinatumiwa kwa kiwango kikubwa katika nchi ya Kenya, Uganda, Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo, Tanzania, Burundi, Rwanda na Msumbiji, Malawi na Zambia

Matumizi ya lugha ya Kiswahili katika mtangamano wa SADC yanaambatana na faida mbalimbali kama kutambulisha utamaduni wa lugha Kiswahili ulimwenguni.

Kiswahili kitatambuliwa rasmi katika nchi wanachama 11 ambazo ni Zimbabwe, Angola, Botswana, Lesotho, Swatini, Afrika ya Kusini, Madagaska, Mauritius, Seychelles, Namibia na Comoro. Kwa kuwa lugha inabeba vionjo vya kiutamaduni wa sehemu fulani, faida hii itaambatana na utambulisho wa utamaduni wa wenyeji wa Tanzania kwa katika nchi hizo. Hivyo, kwa kupitia nchi hizo ni wazi kwamba Kiswahili kitaendelea kusambaa ulimwenguni.

Vilvile matumizi ya lugha ya Kiswahili yatarahisisha mawasiliano kwa Watanzania ya katika kutumia fursa zinazopatikana ndani ya SADC. Faida hii iongeza mwingiliano wa taarifa za kimaendeleo katika nyanja za kiuchumi, kiutalii, kiutamaduni, kiteknolojia na kisiasa.

Pia, matumizi ya Kiswahili katika Jumuiya ya SADC yanaiweka Tanzania katika nafasi nzuri ya fursa zinazoambatana na uhitaji wa elimu ya Kiswahili. Hii inahusisha fursa kwa Tanzania kutoa wataalamu wa kufundisha Kiswahili katika nchi wanachama, fursa ya kuuza vitabu vya kufundishia Kiswahili pamoja na nyenzo nyingine za kufundishia Kiswahili kwa nchi hizo.

MAPENDEKEZO

Serikali ya Tanzania iweke mkakati wa kutumia fursa Kiswahili kutumika katika Jumuiya ya SADC, ikiwemo kuongeza uwekezaji katika elimu ya kiswahili kwa kuhamasisha wanafunzi wa Kiswahili nchini ili kwenda kuwa walimu katika nchi wanachama wa SADC, pia kuandaa na kuzalisha nyenzo za kufundishia na kuweka mkakati wa jinsi ya kuzipeleka katika nchi wanachama
.
Tanzania kama kiongozi wa Jumuiya ya SADC, ichukue hatua za kimkakati kutafsiri nyaraka zote muhimu zilizopo katika tovuti ya SADC kwenda lugha ya Kiswahili katika kipindi hiki cha uongozi.

Hii itafungua na kutambulisha lugha ya Kiswahili katika tovuti na mitando ya kijamii ya SADC. Pia, itasaidia nchi zinazozungumza Kiswahili kuelewa na kutumia taarifa muhimu zinazopatikana katika tovuti ya Jumuiya ya SADC.

Kuanzisha au kuongeza kampeni maalumu kwa Watanzania kutumia fursa zipatakanazo katika Jumuiya ya SADC zinazoambatana na lugha ya Kiswahili.

Sisi wananchi kwa dhati tunaipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kufanikisha Mkutano wa 39 wa viongozi wa Jumuiya ya SADC, pamoja na majukumu mapya ya Rais Magufuli na Waziri wa Afrika Mashariki na Mambo ya Nje, Profesa Palamagamba Kabudi kuwa mwenyekiti wa baraza la mawaziri wa jumuiya hiyo.

Mwandishi ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC)


Comments